.........BLOG HII BADO IPO KWENYE MATENGENEZO......

Jumanne, 1 Mei 2012

MAADHIMISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI IRINGA YADODA ,MGENI RASMI RC IRINGA ASHINDWA KUTOKEA


MEI MOSI NA HALI YA MFANYAKAZI WA TANZANIA

...Ongeza kasi unakaribia maisha bora..

MATOKEO KIDATO CHA SITA 2012 YATANGAZWA



Katibu mtendaji Dkt. Joyce Ndalichako leo ametangaza matokeo ya form six,
Shule iliyoongoza ni MARIAN GIRLS ya Bagamoyo.

Pia amepunguza adhabu ya miaka 3 na kuwa mwaka 1, iliyokuwa imetolewa kwa watahiniwa waliobainika kufanya udangayifu wa matokeo ya kidato cha nne ya mwaka 2011.

Jumapili, 29 Aprili 2012

WATANZANIA WATAKIWA KUSHIRIKI PROMOSHENI YA "VUMBUA HAZINA CHINI YA KIZIBO" YA BIA ZA SERENGETI


KAMPUNI ya Bia ya Serengeti (SBL) imewataka watanzania kushiriki kwa nguvu zote katika promosheni ya Vumbua Hazina ya Chini ya kizibo ili kuweza kushinda zawadi mbali mbali.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Masoko wa Kambpuni ya SBL, Ephrahim Mafuru na kusema kuwa SBL imetenga sh. Milioni 783 ambazo zitatolewa kama zawadi kwa washindi wa promosheni hiyo ambayo itafanyika kwa wiki 16 kuanzia Aprili 22.
Mafuru alisema kuwa zawadi kwa wale watakao jishindia zawadi ya bia zina thamani y ash. Milioni 265 zawadi za fedha taslim ni sh. Milioni 383. Alisema kuwa pia watatoa pikipiki 16, Bajaj inane (8) , Jenereta nane (8) na magari matatu aina ya Ford Figo.
Alisema kuwa ili kuweza kuingia katika shindano hilo unatakiwa kununua bia zao, Serengeti, Tusker au Pilsner na kukuta neno lenye tarakimu saba na kulituma kwenda namba maalum ya 15317 na kuingia katika shindano hilo.
Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Push Mobile, Freddie Manento aliipongeza SBL kwa kuiteua kampuni yake kuendesha shindano hilo hasa kwa kuzingatia ubora wa huduma zake.
Manento alisema kuwa kampuni yao ni bora zaidi katika kuendesha zoezi kama hilo na kuahidi kutoa hudima bora kwa wateja wake.
“Ni faraja kubwa kufanya kazi na SBL katika shindano hili kubwa la kuwazawadia wateja wa bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo ya bia, tutafikisha lengo lililowekwa,” alisema Manento.
CHANZO

Jumanne, 24 Aprili 2012

Lulu ‘amwaga’ machozi mahakamani


MSANII wa filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’, amemwaga chozi mahakamani baada ya kubanwa na askari Magereza waliokuwa wakimlinda akipitishwa katikati ya kundi la watu waliofurika mahakamani kusikiliza kesi hiyo ya mauaji inayomkabili.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana ilifurika watu wakiwemo waandishi wa habari huku wapigapicha wakijitahidi kupata picha ya msanii huyo baada ya siku ya kwanza ya kesi hiyo kushindwa kupata picha hiyo. Kesi hiyo inayosikilizwa na Hakimu Rita Tarimo ilikuja kutajwa.

Baada ya kuingia mahakamani huku akilia, kimya kilitawala mahakamani hapo kwa muda huku askari wakijaribu kumtuliza.

Wakili wa Serikali, Elizabeth Kaganda aliiomba Mahakama kuondoa watu wote kwa hofu ya kusababisha vurugu mahakamani hapo.

Kutokana na ombi hilo, Hakimu Tarimo aliamuru watu waliojazana katika chumba hicho kuondoka kabla mshitakiwa hajaondolewa ili kurudishwa mahabusu.

Lulu alifikishwa mahakamani hapo na gari la Polisi aina ya Toyota Hiace akiwa mshitakiwa peke yake huku akilindwa na askari Magereza.

Baada ya kutajwa kwa kesi yake saa tano asubuhi, Lulu aliondolewa haraka mahakamani hapo akitumia gari hilo hilo huku likipiga ving’ora.

Kamishna Haki za Binadamu amtetea Wakili wa kujitegemea, Kennedy Fungamtama, ambaye anamtetea Lulu, aliwatambulisha mawakili wenzake wa utetezi katika kesi hiyo akiwemo Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu, Joaquine De-Mello, Peter Kibatala na Fulgence Masawe.

Kaganda alidai kuwa kesi ilifika mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa na kwamba upelelezi wa shauri hilo haujakamilika.

Aliiomba Mahakama kupanga siku nyingine ya kutaja na ikapangwa Mei 7. Lulu anadaiwa kumwua msanii mwenzake, Kanumba Aprili 7, Sinza Vatican, Dar es Salaam. Yuko mahabusu kwa sababu kesi ya mauaji haina dhamana.
CHANZO

TAARIFA YA CHAMA CHA WAFANYAKAZI WA SEKTA YA HUDUMA ZA MTANDAO WA MAWASILIANO TANZANIA KWA VYOMBO VYA HABARI


Katibu Mkuu wa TEWUTA Junus Ndaro akitoa taarifa kwa vyombo vya habari kwenye ukumbi wa mikutano wa Idara ya Habari Maelezo leo jijini Dar es salaam juu ya matatizo yaliyopo katika makampuni ya Simu n akuhusu punguzp la tozo inayolipwa kwa Tume ya Mawasiliano TCRA katika picha kushoto ni Ahmed Kaumo mjumbe wa kamati ya utendaji ya TEWUTA.


UTANGULIZI

Tanzania Communication Regulatory Authority (TCRA) imeundwa chini ya Sheria Na. 12 ya Mwaka 2003, ikiwa na majukumu ya Utoaji leseni, Usimamizi na Udhibiti wa Taasisi zote za Mawasiliano ya Simu, Posta, Radio na kadhalika.
Katika kutekeleza moja ya majukumu yake TCRA inawajibika kutekeleza yafuatayo:-
-Kusimamia ushindani wa kibiashara kwa lengo la kukuza uchumi.
-Kusimamia huduma kwa wateja.
-Kusimamia huduma bora.
-Kusimamia bei za huduma (tariffs rate).

MAKAMPUNI YA SIMU YANCHUNGUZWE KATIKA ULIPAJI KODI.
Awali ya yote tunakiri kuutambua vema uongozi wa TCRA na majukumu yake, ambayo kimsingi uongozi huo unawajibika kuyasimamia vema majukumu hayo kwa faida ya Watanzania wote, chombo hiki kilipoundwa Watanzania walio wengi walitarajia kuwa kitakuwa na uwezo wa kusimamia bei za Mawasiliano ya Simu, na kuhakikisha Sekta hii ya Mawasiliano ya Simu hapa nchini inastawisha uchumi wa Tanzania.
Ni muda mrefu tumekuwa tukifuatilia kwa ukaribu na kujiuliza ni kweli Makampuni haya ya Simu, hususani ya Kigeni yamekuwa yakilipa Kodi kwa mujibu wa Sheria za hapa Nchini, na je kuna chombo huru ambacho kinatambua idadi ya Simu zilizopigwa ili kiweze kuisaidia TRA kukusanya mapato?, jibu ni hapana.

Chama cha TEWUTA tunawaunga Mkono Waheshimiwa Wabunge walipowasilisha hoja Bungeni kutaka Makampuni haya yalipe Kodi na kuhakikisha yanazingatia Sheria zote hapa nchini.
Iwapo Makampuni ya Simu hapa nchini yataachwa yatoe Taarifa za Makusanyo ya Fedha, na pasipo kuwepo na chombo cha kuhakikisha ukweli wa taarifa hizo, tutambue kuwa nchi itakuwa inapoteza fedha nyingi ambazo zingezalishwa kupitia Mawasiliano ya Simu.

Ulipaji wa Kodi ni muhimu sana kwa Ustawi wa Nchi, tusingependa kuona Makampuni ya Simu yanakwepa ulipaji wa Kodi au kuwa Sehemu ya uzalishaji mdogo wa fedha za Kodi kutoka sekta hii ya Mawasiliano.
Sote tunatambua wazi kwamba, Makampuni haya yamekuwa yakizalisha fedha nyingi, pamoja na kuwa na idadi kubwa ya wateja, tarajio letu ni kuona yanalipa Kodi kwa uhalisia bila kuwepo kwa uchakachuaji wa aina yoyote.

Tunaitaka TCRA kuisaidia Serikali ili kuhakikisha Makampuni haya yanalipa Kodi halali, ikizingatiwa kwamba hili ni jukumu mojawapo kati ya majukumu kadhaa yanayotakiwa kufanywa na TCRA katika usimamiaji sekta ya mawasiliano hapa nchini, na iwapo TCRA itasimamia vema zoezi hili Makampuni yote yataweza kulipa Kodi na Sekta hii ya Mawasiliano itakuwa ni sehemu yenye mchango mkubwa katika kukuza uchumi hapa nchini.


TOZO INAYOLIPWA TCRA NA MAKAMPUNI YA SIMU NCHINI IPUNGUZWE.
Watanzania walio wengi walitarajia kuwa baada ya kuundwa kwa Mamlaka ya Usimamizi wa Mawasiliano (TCRA) itasimamia na kuhakikisha gharama za huduma za mawasiliano ya Simu zinapungua na kuwa na uwiano sawa kwa tozo la Makampuni yote hapa nchini.
Mamlaka imeshindwa kuwaeleza Wantazania kwa uwazi, na huku ikitambua kuwa moja ya jukumu lake ni kupanga bei elekezi (Harmonize price) kwa Makampuni ya Simu, kitendo ambacho hakijafanyika toka Mamlaka iundwe na kutangazwa kwenye vyombo vya habari.

Ni ukweli kuwa Watanzania wamechoka kutembea na simu zaidi ya moja za Mitandao tofauti, kwa sababu ya kutafuta punguzo kwa Mtandao husika, hii hali tutaendelea nayo hadi lini? Hivi ni kweli hakuna Sheria ambazo zitawalazimisha Wamiliki wa Mitandao kuwa na bei zenye uwiano wa karibu, jibu Sheria zipo. Mbona TCRA imelala na kuona Watanzania wananyonywa hadi Senti yao ya Mwisho, tunapaswa kuwajibika.

Ni lazima mtambue kuwa uudwaji wa Chombo hiki ni kumsaidia mtumiaji (Mteja) asinyonywe na iwapo TCRA inasahau majukumu yake, Watanzania wataendelea kuilalamikia Serikali. Wakati sasa umefika wa kusema hapana, kila chombo kiwajibike na kuhakikisha wanaisaidia Serikali ili kuleta utulivu Nchini.
Rejea historia ya nyuma, Wamiliki wa Mitandao walikuwa na hoja ya msingi ya kwamba gharama za uedeshaji wa shughuli za mawasiliano zilikuwa juu sana kwa sababu Mawasiliano yaliwezeshwa kwa kupitia kwenye Satellite, lakini hivi sasa Serikali imetuletea Mtandao wa Mkongo (FIBRE) ambao gharama zake za uendeshaji ni ndogo sana na unafanya kazi vizuri kwa haraka zaidi.
Hivyo basi uwezekano mkubwa wa kupunguza gharama za mawasiliano hapa nchini upo.TCRA katika kuhakikisha kwamba gharama za mawasiliano zinapungua kwa sasa ni lazima ikubali kupunguza gharama zake.
TCRA inapaswa kufanya kama ifuatavyo:-
TCRA inapaswa kusitisha malipo ya Tozo ya maunganisho (Interconnection rate) yanayolipwa kwa fedha za Kigeni (DOLA) kwa Makampuni ya Simu, pia kiwango kinachotozwa bado ni kikubwa na kinapaswa kuondolewa au kupunguzwa kwani hakina faida kwa mtumiaji.

TCRA inapaswa kuondoa au kupunguza gharama za viwango vya kupiga simu (Tarriff) kwa Makampuni yote ya Simu hapa nchini ili kuwa na gharama elekezi.

TCRA inapaswa kupunguza gharama za malipo (TOZO) ya umiliki wa njia za Mawasiliano (Frequency) inayolipwa kwa fedha za kigeni na kiwango kilichopo ni kikubwa.
TCRA inapaswa kupunguza Malipo (TOZO) inayoyatoza Makampuni ya Simu kama gharama za malipo ghafi kwa mwaka (Loyalty fee), ni ukweli kiwango hiki cha asilimia 0.8 ni kikubwa na kinasababisha watumiaji kuumia.

TCRA inapaswa kupunguza gharama za Malipo ya Mawasiliano Vijijini (Rural areas) ya asilimia 0.4 yanayotozwa Makampuni ya Simu.

TCRA inawajibika kutambua idadi ya Simu zote zinazopigwa kutoka Mtandao Mmoja kwenda Mwingine, hili ni jukumu lao na hatukubaliani na Mawazo ya kutafuta Kampuni nyingine ili kufanya kazi hiyo, hayo ni mawazo ya Kifisadi na hayakubaliki.

Kwa kuwa TCRA inaonyesha dhahiri kujali kukusanya fedha tu, na kuacha majukumu yake ya msingi, tunadhani sasa ni muda muafaka wa Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia kuandaa Mswada na kuufikisha Bungeni ili Malipo yote yanayolipwa TCRA yakusanywe na TRA, iwapo Mheshimiwa Waziri atatekeleza hili TCRA itakuwa na nidhamu ya kusimamia maslahi ya Nchi.

Iwapo TCRA haitatekeleza haya kamwe Watanzania wasahau kwamba kuna siku moja gharama za Simu zitapungua, Chombo kilichoaminika na Serikali katika kudhibiti bei ndio chanzo kikubwa cha upandaji wa bei za gharama za Simu.
Ni lazima tutambue kuwa Uwepo wa Chombo hiki ni kudhibiti bei kwa watumiaji na kuhakikisha Makapuni yote yanakuwa na bei elekezi zenye uwiano mmoja.
Mwisho, tumechoka kubeba Simu nyingi za kila Mtandao tunaitaka Bodi ya TCRA pamoja na uongozi wa TCRA kukutana ili kujadili Bei na kuhakikisha inawapunguzia watumiaji bei pamoja na Makampuni husika.

Imesithibitishwa
JUNUS P. NDARO
KATIBU MKUU TEWUTA
SIMU: 0732 – 200222
0786 – 200224

Imetolewa na kusoma leo tarehe 24 /04/2012 saa tano asubuhi .
CHANZO

ASKARI POLISI WANNE WAFUKUZWA KAZI KIGOMA KWA KUDAI NA KUPOKEA RUSHWA

JESHI la Polisi mkoani Kigoma leo limewafukuza kazi askari wake wanne kwa tuhuma za kudai na kupokea rushwa ya dola 300 za Kimarekani kutoka kwa raia mmoja wa China kinyume na maadili ya Jeshi hilo.

Kamanda wa Polisi mkoani Kigoma Frasser Kashai amewataka mwenye namba E.3890 CPL Admirabils Malaso(43), G. 814 PC Waziri Juma Rashidi(30) G. 3012 PC Makasi Edwin(25) na G. 3322 PC Elias Zakaria(24) ambao wote walikuwa wakifanyia kazi katika kituo cha Polisi Uvinza wilaya ya Kigoma Vijijini.

Kamanda Kashai amesema kuwa mnamo Aprili 1, 2012 majira ya saa 5.00 usiku askari hao wakiwa zamu katika kituo hicho cha Polisi Uvinza, walipokea taarifa kwa njia ya simu ya mkononi kutoka kwa dada mmoja aitwaye Mary Kapele(26) akiwaeleza kuwa yuko katika nyumba moja ya kulala wageni ya Manchester na alikuwa na Raia mmoja wa Kichina mmoja wa wasimamizi wa ujenzi wa barabara ya kutoka Kigoma Uvinza na kwamba waende kumshika ugoni ili wajipatie fedha na baadaye kugawana na dada huyo.

Askari hao walikwenda katika nyumba hiyo ya kulala wageni na kumkamata Mchina huyo aitwaye Mafutao War, akiwa pamoja na dada huyo kisha wakamtaka atoe fedha kama malipo ya kumshika ugoni na ndipo walipopewa kiasi cha dola 300 za kimarekani na shilingi 10,000 za Kitanzania na kumuachia. Kamanda kashai amesema kuwa mlalamikaji Bw. War alikuwa ni mkandarasi wa ujenzi wa barabara ya Kigoma Uvinza.

Kamanda Kashai alisema baada ya kuona tukio hilo, raia wema walitoa taarifa Polisi mkoani Kigoma ambapo askari hao walikamatwa na baada ya uchunguzi kufanyika walibainika kuwa walihusika na tukio hilo na ndipo waliposhitakiwa kijeshi na kupatikana na hatia ya kufanya Kitendo kibaya kinyume na mwenendo mwema wa Jeshi la Polisi.

Amesema kufuatia hukumu hiyo ameamua kuwafukuza kazi kwa fedheha ili iwe fundishi kwa askari wengine kufuata utaratibu na sheria katika utendaji wa kazi zao za kila siku.

Kamanda Kashai amesema Koplo Admirabils Malalo ambaye alizaliwa Julai 1, 1969 katika kijiji cha Kilando wialaya ya Nkasi mkoani Rukwa, alijiunga na Jeshi la Polisi Julai 26, 1991 na hadi anafukuzwa amelitumikia Jeshi hilo kwa muda wa miaka 11, Kostebo Waziri Juma Rashidi alizaliwa Julai 1, 1982 katika kijiji cha Maisaka wilaya ya Babati mkoani Manyara, na alijiunga na Jeshi la Polisi Februari 05, 2007 na hadi kufukuzwa kwake alikuwa amelitumikia Jeshi la Polisi kwa muda wa miaka mitano.

Amesema Konstebo Makasi Edwin ambaye alizaliwa Februari 28, 1987 huko kwenye eneo eneo la Mabatini mjini Mwanza la na kujiunga na Jeshi la Polisi Juni 28, 2009 amelitumikia Jeshi hilo kwa muda wa miaka mitatu na Konstebo Elias Zakaria ambaye alizaliwa mwaka Julai 1, 1988 huko katika eneo la Nguvumali mjini Tanga na alijiunga na Jeshi la Polisi Juni 28, 2009 ambaye naye pia amelitumia Jeshi hilo kwa muda wa miaka mitatu tu.

Kamanda kashai amesema kuwa Jeshi la Polisi halitasita kumchukulia hatua kali za kisheria na hata kumfukuza kazi askari yeyote atakayebainika kwenda kinyume na maadili ya Jeshi hilo iki ni pamoja na kujihusisha na vitendo vya utovu wa nidhamu, uhalifu ukiwemo wa kudai na kupokea rushwa.

Pinda aziba masikio mawaziri kujiuzulu



ALIPOULIZWA AKACHEKA, MKONO NAE AWEKA SAINI AONDOLEWE, UFISADI MALIASILI UNATISHA

WAKATI wabunge wakiendelea kusaini fomu ya majina ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kiongozi huyo wa shughuli za Serikali bungeni jana alikwepa kuzungumzia hatua za kinidhamu dhidi ya mawaziri wanaokabiliwa na tuhuma mbalimbali.

Akiahirisha Mkutano wa Saba bungeni Dodoma, Pinda hakugusia suala la kujiuzulu kwa mawaziri wanane na badala yake alisema: “Siku zote Serikali imekuwa tayari kupokea ushauri wa Bunge baada ya kusikiliza mjadala na mapendekezo ya waheshimiwa wabunge.’’

Baada ya kuahirishwa kwa Bunge hadi Juni 12, mwaka huu. Pinda akiwa nje ya Bunge alikwepa kuzungumzia suala hilo licha ya kubanwa na waandishi wa habari na badala yake alicheka: "Haahaa," kisha akaingia kwenye gari na kuondoka.

Kiongozi wa Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema kitendo cha Pinda kushindwa kuzungumzia chochote kuhusu agizo la wabunge kutaka mawaziri wanane wawajibishwe, kimewaacha wananchi katika hofu.

Alisema Waziri Mkuu ametoa hotuba nyepesi kama vile taifa haliko katika giza kutokana na Bunge kutaka kuwajibishwa kwa mawaziri hao na kuapa kulifikisha suala hilo kwa wananchi.

“Aliahirisha shughuli za Bunge kama hakuna kitu kikubwa kilichohitaji majibu ya Serikali, wananchi walitaka kusikia mawaziri waliotajwa kwa tuhuma za ufisadi wakiwajibishwa lakini, hakuna chochote kilichofanyika. Sasa sisi tutakwenda kwa wananachi.

Jumamosi iliyopita, Pinda aliahidi kuwa jana Serikali ingeweka hadharani msimamo wake kuhusu suala baadhi ya mawaziri kutakiwa kujiuzulu lakini hakutekeleza ahadi yake.

Jana, Waziri Mkuu alisema Serikali itachukua hatua stahiki kuimarisha usimamizi na utendaji ndani ya wizara, Serikali za Mitaa na vyombo husika katika kuhakikisha watendaji wake wanafanya kazi kwa umakini.

Mhe. Mkono alamba sahihi kwenye karatasi ya Zitto




Juzi usiku Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (Nec) na Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono, juzi usiku alisaini fomu ya majina ya wabunge wasiokuwa na imani na Waziri Mkuu yanayokusanywa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto kabwe.

Zitto alikuwa akikusanya saini za wabunge wasiopungua 70 ambao ni asilimia 20 ya wabunge wote ili awasilishe hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu kwa Spika wa Bunge.

Mkono alikuwa ni mbunge wa 74 na wa sita wa CCM kati ya 76 waliosaini fomu hiyo hadi jana mchana. Juzi usiku, Mkono alimpigia simu Zitto na kumtaka ampelekee fomu hiyo ili aweke saini yake.

“Mimi ni mjumbe wa NEC na nimepata nafasi hiyo kwa kuchaguliwa na wabunge wenzangu wa CCM, sasa ninapoona wabunge wenzangu wakiwemo wa CCM wanalalamikia utendaji wa mawaziri wetu kwa kuhusishwa na ufisadi wa fedha za umma na Serikali inakaa kimya ni lazima nichukue hatua,” alisema na kuongeza:

“Mawaziri wetu hata wafanye kosa gani sisi wabunge hatuwezi kuwawajibisha, ni mmoja tu naye ni Waziri Mkuu ambaye tunaweza kufanya hivyo. Sasa tumeona kuna mawaziri wamekutwa na kashfa mbalimbali na bado wanang’ang’ani kubaki kwenye nafasi zao hatuna jinsi, ili kuwang’oa nilazima tumuondoe Waziri Mkuu.”

“Sina tatizo na Pinda katika utendaji wake wa kazi lakini hatuwezi kuwaondoa mawaziri wenye kasoro bila ya kumwondoa yeye kwa mujibu wa sheria zetu, ndiyo maana nimesaini fomu hii kwa maslahi ya taifa langu.”

BWENI LA WANAFUNZI LATEKETEA KWA MOTO HANDENI


WANAFUNZI takriban 50 wa Shule ya Sekondari Kidereko wilayani Handeni hawana sehemu ya kujihifadhi baada ya bweni lao kuteketea kwa moto pamoja na baadhi ya vifaa vyao vya shule.

Bweni hilo liliteketea kwa moto hivi karibuni majira ya asubuhi baada ya kutokea kwa hitilafu ya umeme kwenye bweni hilo muda ambao wanafunzi wote walikuwa wakiendelea na masomo darasani.

Akizungumza eneo la tukio Mwalimu wa Taaluma wa shule hiyo, Khamis Said amesema vitu vyote vya wanafunzi takribani 50 waliokuwa wakiishi katika bweni hilo viliteketea kwa moto, yakiwemo madaftari ya wanafunzi, nguo, magodoro na vitanda vya mbao viliteketea kwa moto.

“Hatukufanikiwa kuokoa kitu maana baada ya kusikika mlipuko na baadhi ya watu kuona moshi ukitoka ndani ya bweni hilo ambalo muda huo lilikuwa limefungwa tulikuta moto umesha tanda ndani na ukiwaka kwa kasi jambo hali ambayo ilikuwa ngumu kuokoa,” alisema Said.

Amesema kwa sasa wanafunzi hao wanasaidiwa na wanafunzi wenzao kimalazi huku wakiishi kwa shida kutokana na msongamano uliopo baada ya bweni lao kuteketea kwa moto. “Unajua baada ya ajali walibaki na nguo za shule walizokuwa wamevaa siku hiyo pamoja na madaftari ya vipindi vya siku hiyo tu, vifaa vingine vyote viliteketea kwenye ajali hiyo…shule imetoa baadhi ya fedha na kuwanunulia maitaji kadhaa japokuwa hayatoshelezi” alisema Mwalimu Said.

Hata hivyo alisema tayari uongozi wa idara ya elimu wilaya ya Handeni umetembelea eneo la tukio na wanafanya utaratibu wa kuwasaidia wanafunzi hao. Hii ni mara ya pili kutokea kwa majanga ya moto shuleni hapo kwani mwaka 2000 wanafunzi walichoma ofisi ya Mkuu wa Shule hiyo baada ya kuzuka kwa vurugu kati yao na uongozi wa shule.

Habari hii imeandaliwa na mtandao wa habari: www.thehabari.com